AZIMIO LA KUPINGA KUPITISHWA KWA MUSWADA WA MAREKEBISHO YA SHERIA NAMBA 3 YA MWAKA 2020
AZIMIO LA KUPINGA KUPITISHWA KWA MUSWADA WA MAREKEBISHO YA SHERIA NAMBA 3 YA MWAKA 2020
Why this petition matters
AZIMIO LA KUPINGA MUSWADA WA SHERIA NA KUTAKA BUNGE KUTOPITISHA MUSWADA HUO UNAOLENGA NA KUCHOCHEA UKIUKWAJI WA KATIBA YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
Ndugu RAIA MWEMA,
Awali ya yote tunakushukuru na kukupongeza kwa kazi kubwa ya kuzuia kuenea kwa COVID-19 hasa wakati huu ambapo dunia inaendelea kupambana na janga la virusi vya Corona (COVID 19).
Ndugu RAIA MWEMA,
Mtandao wa Wanaharakati Tanzania yaani Tan-Act pamoja na Asasi za Kiraia (CSOs) tumesikitishwa na kitendo cha MWANASHERIA MKUU wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufanya maamuzi yanayokiuka misingi ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kupendekeza Muswada wa Mabadiliko ya Sheria mbalimbali ambazo baadhi zinakiuka Misingi ya Katiba ya nchi.
Itakumbukwa kwamba, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi ya Kidemokrasia ambayo moja ya msingi wake mkuu ni Utawala wa Sheria na Haki Za Binadamu.
Kwa mujibu wa Katiba na sheria zingine za nchi, Ibara ya 13 Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaeleza wazi kwamba Watu Wote ni Sawa mbele ya Sheria na pia Ibara ya 8 ya KJMT inatamka wazi kwamba Wananchi ndio msingi wa Mamlaka yote. Hivyo ni marufuku kutunga sheria ambayo inabagua RAIA wa nchi hii na kuwapora Haki na Mamlaka yao ikiwemo Haki ya kutumia Mahakama wakati wowote wanapohisi kuvunjiwa Haki zao.
Ndugu RAIA MWEMA,
Kitendo cha MWANASHERIA MKUU wa SERIKALI kukusudia kuwasilisha Bungeni Muswada wa Mabadiliko ya Sheria mbalimbali ikiwemo mapendekezo yanayokusudia kuminya haki ya RAIA wa Tanzania kutumia Haki za Kikatiba pindi wanapoona dhahiri Haki za Kikatiba zinapuuzwa au kuvunjwa na pia kukusudia kuwawekea Kinga za kutokushtakiwa kwa baadhi ya Raia kwa sababu ya nyadhifa na vyeo vyao ni ukiukwaji wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa kuwa Katiba inatamka wazi katika Ibara ya na 13(5) kuhusu marufuku ya ubaguzi.
Na kwa kuwa kila RAIA ana wajibu wa kusimamia na kutetea Katiba na Sheria, sisi kama Mtandao wa Wanaharakati Tanzania chini ya Uratibu wa CILAO tunaomba kushirikiana nawe na wadau wengine kusaini azimio hili la haraka ili kumtaka MWANASHERIA MKUU wa SERIKALI kubatilisha maamuzi yake na kwa haraka iwezekanavyo tushirikiane kupinga na kuwaomba Wabunge kutoruhusu kujadili na kupitisha muswada huu ambao ni sumu kwa Haki za Binadamu nchini.
#PamojaTulindeKatiba
Imetolewa na:
Mtandao wa Wanaharakati Tanzania (Tanzania Network of Activists - TanAct )
Decision-Makers
- Asasi za Kiraia
- Mahakama za Tanzania
- Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
- Mtandao wa Wanaharakati Tanzania
- Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania